BISHOP: KWANINI NIGERIA IWE KIPIMO CHA FILAMU ZETU?



Sekta ya filamu Tanzania kwa sasa inajulikana duniani licha ya matatizo yake, licha ya mtayarishaji wa filamu wa Tanzania kuendelea kuishi maisha yasiyo tofauti na mtu mwingine wa kawaida! Hali halisi ya soko la filamu nchini inabana sana uwezekano wa kuibuka kwa wasanii, watayarishaji au waongozaji wapya...

Sidhani kama kuna mtu atabisha kuwa filamu za kibongo ‘hazitesi’ katika ukanda wa Afrika Mashariki na maeneo ya Maziwa Makuu. Filamu hizi zimesaidia kwa kiwango fulani kuitangaza nchi hii, kuwatangaza wasanii wa nchi hii, lakini vipi kuhusu maisha ya wasanii hawa? Je, wanapata stahili yao na wanaishi kwa kutegemea filamu pekee?

Kinachosikitisha zaidi: utoaji wa hizi filamu zetu imekuwa kama mchezo wa soka bila refa, sawa na mkutano bila mwenyekiti, darasa bila mwalimu, au nyumba (familia) bila mzazi…

Wafanyabiashara wanaahidi milioni kumi na tano hadi ishirini na ushee kwa sinema; watoaji sinema wanalipua kazi; waigizaji hawalipwi vizuri; utengenezaji sinema unafanywa haraka haraka. Sinema zinatengenezwa kwa wiki moja na zinatolewa ndani ya mwezi mmoja tu. Haraka haraka…

Wasanii wa filamu wanaigiza bila script wala mazoezi, watengenezaji filamu wengi wanatumia mwanya huo kula uroda na wasichana wazuri wazuri (ndiyo maana siku hizi kuwa miss ni kigezo kikubwa cha kupata nafasi ya kucheza filamu, haijalishi kama una kipaji cha kuigiza au la), sinema zinazotolewa nchini eti zinalinganishwa na za Wanaijeria! Tangu lini sinema za Wanaijeria zikawa kipimo cha filamu?

Kwa nini tufuate nyayo za Nollywood katika kuzalisha sinema zetu? Kwa kipi hasa? Hii inatufanya kusimulia hadithi zao; angalia sinema zetu zinavyosimulia uchawi, zinavyosimulia mapenzi au mikasa ya kijamii utagundua hilo. Tunaiga hadithi zao, namna yao ya uchezaji, sinema zao ambazo nyingi zimekuwa zikiigwa kutoka mataifa ya Magharibi na India.

Hivi Watanzania tumelogwa? Hii ni kwa Watanzania wote. Kwanini hatupendi/ hatununui sinema zinazotolewa na Watanzania wenzetu? Kisa? Hazituvutii. Moja ya sababu ni kwamba zinatengenezwa vibaya kwa kulipuliwa. Lakini kwa nini hata sinema zinazotengenezwa vizuri bado hatuzinunui? Kwa nini hatuzifurahii? Kwa nini hatuzitolei maoni na kuzitangaza? Tunachoweza ni kuziponda tu! Hivi hatudhani kuwa hiyo ndiyo njia kuu itakayotufanya tuendelee kama wenzetu, tunaowaona Miungu kutuzidi?

Kwa upande wa waandaaji wa filamu tukumbushane kwamba sinema ni sanaa inayochukua muda. Hatuwezi kutengeneza sinema ikakamilika ndani ya mwezi mmoja tu. Tujipe muda katika kuifanya kazi kwa ufanisi zaidi. Ingawa wapo wanaosema kuwa sababu ya kufanya kazi haraka haraka ni kutokana na matatizo ya pesa ambapo mtu huhitaji kupata pesa haraka ili atatue matatizo yake. Lakini tunasahau kuwa ukitoa kazi nzuri yenye ubora hukaa na huuzika miaka nenda miaka rudi, tofauti na kazi zetu ambazo baada ya wiki mbili zinakuwa hazina tena soko.

Tukumbushane kujipa muda katika uandaaji wa filamu zetu: Mwezi mmoja wa mikutano kupanga mambo (wapi itapigwa picha, nani atafanya nini, waigizaji watatoka wapi, watafanya nini), mwezi mwingine kupanga usanii (mazoezi ya waigizaji, mazingira yao), mwezi mwingine wa kupiga picha. Baada ya miezi mitatu, mingine miwili ya kuhariri na kusahihisha makosa.

Ndipo sasa kifuate kipindi cha kuitangaza kusudi iuzwe. Ukichunguza sana utagundua kuwa sinema haiwezi kumalizika chini ya miezi sita kwa mazingira ya Tanzania. Ndiyo maana wenzetu wanatoa sinema moja tu kwa mwaka lakini pesa wanazopata wanakula kwa miaka kibao. Sisi tunatoa sinema kila mwezi lakini pesa yake ni ya kujikimu tu.

Ni wakati sasa umefika tushirikiane, tuzichangamkie na tuangalie sinema zetu, tuzifurahie na tupeane moyo…

  • Goddy Semwaiko Asante kwa mawazo mazuri na mchango mkubwa wa ushauri.
    Kuhusu kutonunua Video za Bongo (Hata siku moja sintaziita Filamu, kwani si filamu)
    Bishop inakuwa ngumu kununua kitu kisichokuwa na ubora, na hata ikitokea mojawapo ina ubora, inakuwa ngumu kuigu
    ...See More
  • Goddy Semwaiko Kama Music Video ya dakika 4 inatengenezwa kwa ubora, wasanii wanahangaika mpaka wanasafiri nje ya nchi kutafuta ubora, inakuwaje Video za maigizo za dakika 90-120 zisitengenezwe kwa ubora?
    Nadhani wanaweza kupiga mahesabu vizuri tu na kujipanga.
  • Coletha Raymond kaka upo?????????mbona kimya sana???????????hatutafutani????

Posted by bongofilmdatabase on 8:58 PM. Filed under . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0

0 comments for BISHOP: KWANINI NIGERIA IWE KIPIMO CHA FILAMU ZETU?

Post a Comment

LETS HOOK UP

.

.
.
slide

SIRI YA MTUNGI PHOTO CAPTION


Recently Commented

ALBUM YA BONGOFILM

SIMULIZI ZILIZOBAMBA KWENYE KURASA ZA KIJAMII

TAKE ONE -HBABA NA FLORA INTERVIEW

2009 Bongofilmdatabase. All Rights Reserved. - Designed by Oscar kwa ushirikiano wa SimplexDesign